Munishi
Group:
Members Posts: 77 Joined: Nov. 2003
|
 |
Posted: Dec. 08 2003,12:36 |
 |

KATIBA
SIYO MALI YA CCM
http://munishi.com/
Katiba ya
Tanzania ni ya watanzania. Siyo mali ya CCM. Lazima kila mtanzania
ahusike katika kuirekebisha au kuibadili. Kuna mengi yanayohitaji
marekebisho na mengine yatatolewa kabisa. Najua kwamba nikiingia
ikulu na katiba ya sasa itanikwamisha mengi. Tanzania ni sawa na
gari iliyonoki injini. Inataka matengenezo kamili ndani ya
injini. Siwezi kuifanyia Tanzania MAREKEBISHO INAYOSTAHILI bila ya
katiba mpya. Hata kama kipengele kimoja kitabadilishwa niweze
kugombea bila chama cha kisiasa, hilo siyo lengo langu.
Lengo
langu ni kuleta mabadiliko ambayo ndiyo kiu ya watanzania wengi
wakubwa kwa wadogo. Hatuwezi kuwa na nchi yetu, bila katiba yetu.
Tena katiba haiwezi kuwa yetu kama haina mchango wa mawazo yetu.
Tunahimiza zoezi la kukusanya mawazo kutoka kwa watanzania wote
lianze ndipo katiba irekebishwe. Bila hilo kufanyika hakuna
sababu ya kufanya uchaguzi kwani CCM watatumia mapungufu yaliyoko
kwenye katiba kushinda uchaguzi kiulaini.
Tumeliona hilo.
Ndiyo maana tunasema kwamba hakuna aliyehitimu kuingia katika
uchaguzi na katiba ya sasa. Ina mapungufu mengi, Hatuitaki, Ni
batili. Yeyote atakaeingia kwenye uchaguzi na katiba ya sasa ajue
anafanya hivyo kinyume cha sheria. Ndiyo ni kinyume cha sheria kwa
sababu Watanzania wengi wanataka KATIBA MPYA. Kujaribu kuwaburuza
ili waingie kwenye uchaguzi bila ya kuibadili katiba ni mbaya kuliko
wao kuchukua silaha na kuanza kudai haki zao kwa mtutu wa bunduki.
Hatuombi hali ifikie hapo kwani itatuumiza wote. Lakini ikibidi,
Hakuna jinsi.
Kuhusu baraza la mawaziri, nilisema wazi kwamba
mimi sitakuwa na uwezo wa kuunda baraza la mawaziri. Katiba ya sasa
inamruhusu rais kuunda baraza lake la mawaziri. Katiba mpya
italiruhusu bunge kuunda baraza letu la mawaziri. Sifa za
watakaogombea nafasi za uwaziri lazima ziambatane na taaluma zao
katika wizara husika. Wakati wa kuchaguliwa waziri kwa sababu za
kikabila, kiundugu na kirafiki, UMEKWISHA. Hata hapa kuna wengi
tayari nimeona wataifaa Tanzania katika baraza la mawaziri. Mtu kama
Augostino Moshi ukisoma posti zake utaona uanasheria ndani yake.
Hawa ndio tunaotaka kuwahimiza wagombee nafasi za waziri wa
sheria na katiba. Wabunge wakiridhishwa na kuhitimu kwao katika fani
husika watawachagua. Nimemtaja Moshi siyo kwa sababu ni mchagga,
bali nipate nafasi ya kujibu swali lake. Aliniuliza kama nakimudu
kiingereza. Ukweli ni kwamba kiingereza nakimudu
vizuri.
Lakini nilijifunza kwa njia ngumu zaidi. Nikija
Nairobi mwaka 1984 nilikuwa siwezi kabisa kuwasiliana kwa
kiingereza. Jambo hilo lilinikera sana. Niakaamua kuanzia mahali.
Biblia ndicho kitabu kilichokuwa hakibanduki mikononi mwangu.
Nilikuwa nimemaliza kuisoma na kuirudia mara tatu. Nikanunua
madaftari makubwa ya kuandikia kama matano, halafu nikanunua Biblia
ya kiingereza. Nilianza kuandika neno hadi neno, nikamaliza kuandika
agano jipya. Mengi nilielewa maana kutokana na ukweli kwamba
nilikuwa nimeyasoma katika Biblia ya kiswahili. Yaliyonishinda
matamshi ilinibidi ninunue biblia katika kaseti. Yale ambayo
sikuelewa kuyatamka, Biblia ya kaseti ilinisaidia kujua yanatamkwa
vipi.
Hata kabla ya kumaliza agano la kale tayari nilikuwa
na kiingereza kingi sana akilini mwangu. Tayari niliweza kuwasiliana
kwa kiingereza kuliko. Nasita kusema kuliko wasomi wengi
Tanzania, lakini ukweli unabaki hivyo. Sasa hivi ndipo kasi ya
kujifunza kiingereza imeongezeka Tanzania. Wakenya na Waganda
wamefungua shule uchwara na wanaziita za kimataifa kwa sababu tu
wanazingatia somo la kiingereza. Ningekuwa najua kutumia kompyuta
wakati huo, nisingepitia njia ngumu hivyo kukijua kiingereza.
Lakini sijuti kwani maneno mazito ndani ya Bibilia
yamekiongezea uzito kiingereza ninachotumia kuzungumza na hata
kuandika. Sitaki nijisifu kwamba Kiingereza changu ni sawa na kile
cha malkia wa UINGEREZA, lakini nitakuwa mpumbavu gani nishindwe
kujieleza kwa lugha rahisi kuliko zote duniani? Kiingereza kwa sasa
ndiyo lugha rahisi kuitumia kuliko hata kiswahili. Haya
niliyoyaandika hapa hakuna mahali katika kompyuta naweza
kufanya "SPELL CHECKING", sababu ni kiswahili. Lakini ingekuwa
kiingereza, bila kujali natumia programu gani nitapata mahali pa
kuisahihisha kazi yangu kiulaini.
Ni urahisi huo ndio
unaonipa mashaka kwamba wengi hawajui kiingereza. Kuna rafiki yangu
simtaji. Ni mwandishi wa habari katika gazeti la NATION
lichapishwalo kwa kiingereza kila siku nchini Kenya. Ukisoma makala
zake, utapenda. Mpangilio wa lugha, usahihi wa maneno, NK. Lakini
wacha akuandikie barua ya mkono, Au akutumie ujumbe mfupi kwa simu
za kipepesi. Utashangaa mbona kiingereza chake kibovu? Kumbe
amelemazwa na kompyuta ambayo inamfanyia kila kitu kuanzia "SPELL
CHEKING" mpaka na mtiririko wa lugha. Je ni kitu cha kujivunia kujua
kiingereza? Hapana. Hata wanaokiongea au kukiandika vibaya siyo
makosa yao. Siyo lugha yao ya kwanza maishani.
Pamoja na
umuhimu wa kiingereza duniani leo, Siungi mkono kasi watanzania
waliyo nayo katika kukikimbilia kiingereza. Wengi wanalipa pesa za
kutisha kwenye shule ambazo zinatilia mkazo kiingereza, Wengine
wanawapeleka watoto wao nje Kenya Uganda, Na hapo nimetaja sehemu
chache sana. Yote ni watoto wajue kiingereza. Kuna tofauti kati ya
kuelimika na kujua lugha. Lakini kwa watanzania wengi hilo
hawalijui. Wanafikiri kuelimika ni kujua Lugha. Kuna uwezekano wa
kuzijua lugha tofauti bila kuwa na elimu. Lakini kiingereza tu,
sioni ulazima wa wazazi Tanzania kwenda kasi wanayokwenda
kukifukuzia kiingereza. Kuna njia nyingi za kuweza kuijua lugha
yeyote bila kuingia gharama kubwa wanazoingia watanzania.Nimalize
kwa kusema kuna njia nyingi za kumuua panya. Ukiweka mtego utamnasa
atakufa. Ukiweka dawa ya sumu jikoni, panya atakula na atakufa.
Lakini ole wako mtoto wako akidhani hiyo uliyoweka jikoni ni
peremende. Uliyotarajia yampate panya yatampata mtoto wako.
Watanzania wengi wameamua kumuua panya wa kiingereza
wakitumia sumu jikoni. Tayari nimeiona hatari mbele yao. Nani
awaambie njia nyingine rahisi ambayo ni kumchagua Munishi awe rais
wa Tanzania chini ya katiba mpya nitainua kiwango cha elimu. Kiwango
cha elimu kikiinuka Lugha zozote hazitakuwa ngumu watanzania
kuzitumia. Naujua ugumu nilioupata kujua niyajuwayo, sitopenda mtoto
wa kitanzania apitie niliyoyapitia kupata elimu.
Bwana Moshi
nafikiri nimekujibu. Nashukuru kuniuliza hilo, kwani CCM wamekuwa
wakimtesa sana Mrema kwa hilo. Najua hata mimi wataanza kutumia hilo
kama mtaji wa kunipinga nisiwe rais. Lakini hata Mkapa kiingereza
chake ni cha kubabaisha pamoja na kwamba alisomea lugha ya
kiingereza kama somo ili aweze kuwa mhariri wa DAILY NEWS. Kwa mtaji
wa lugha tena ya kiingereza hapa wamefika. Watafute jingine. Ikulu
nitaingia tu. Nia na sababu ninazo. Kama walifikiria kwamba uwezo ni
kiingereza, basi hata uwezo ninao.
Kuhusu swali la
uraia, maoni yangu ni kwamba Mtanzania anayetaka kurudi kuuchukua
uraia wake, itabidi aukane uraia aliouchukua ugenini. Ni maoni yangu
binafsi. Lakini kwa sababu tutabadili katiba, sijui maoni ya
watanzania yatakuwaje kuhusu hilo. Kulingana na katiba ya sasa, Rais
anakuwa kila kitu. Ndiyo maana maswali kama utafanyaje kuhusu hili
na lile yanajitokeza kwa wingi. Lakini KATIBA MPYA mambo hayatakuwa
hivyo. Kila jambo litashughulikiwa na wizara husika na wanataaluma
husika.
Swali la uraia litashughulikiwa idara ya uhamiaji.
Katiba mpya itawatengenezea mazingara mazuri ya kufanya kazi yao
bila kuingiliwa kisiasa. Kwanza kutakuwa hakuna chama cha kisiasa
madarakani.
Maswali mengi niliyatarajia, na bado
nayatarajia. Wengi wamezoea sana utawala wa CCM wala hawajui
itakuwaje bila CCM. Mimi naiona Tanzania mpya bila CCM. Picha hiyo
iko akilini mwangu. Niko tayari kuendelea kuwafafanulia zaidi picha
ya Tanzania mpya. Naiona iko nami. Mungu ameiweka maishani mwangu.
Hakuna kitakachonitenga na Tanzania mpya iliyo maishani mwangu,
labda maisha yenyewe ndiyo yanaweza kunitenga na Tanzania mpya na
katiba mpya, halafu MAISHA MAPYA YA WATANZANIA. Mungu bariki
watanzania. Waonyeshe Tanzania mpya bila CCM.
|