13 Next Page   
  Topic: CCM IMESHUSHA JEHANAMU TANZANIA, HOTUBA YA MCHUNGAJI KWA TAIFA < Next Oldest | Next Newest >  
Munishi



Group: Members
Posts: 77
Joined: Nov. 2003

Posted: Dec. 23 2003,13:56   


http://munishi.com/

TANZANIA ILIANZA VIBAYA INAELEKEA PABAYA


Tanzania ilianza vibaya ndiyo maana inaelekea pabaya. Kuanzia wakoloni na Nyerere waliotutawala, Wote waliifanya Tanzania kuanza vibaya. Lazima tuanze upya vizuri, ili tuelekee pazuri. Watanzania tumechoshwa  na sera za kwenye vitabu, lakini kwenye maisha yetu hazitekelezeki. Tumepotezewa muda mrefu ambao tungeutumia vizuri leo hii hali yetu kimaisha ingekuwa tofauti na ilivyo sasa.

Lakini yote hayajapotea kwani tuna muda wa kuanza upya. Hatutakuwa na muda wa kupoteza kwani tayari tumepitwa na wakati. Tutaanzia tutakapoikuta nchi yetu na tuendelee mbele. Muhimu hatutarudia makosa ya zamani. Tutarekebisha yanayoweza kurekebishwa haraka ili angalau tupumue hewa yenye mabadiliko.

Tutaanza na kodi. Wananchi watapunguziwa mzigo wa  kodi, na  tutabadili mfumo wa kuikusanya. Tofauti na ilivyo sasa kodi kidogo sana itatozwa katika bidhaa muhimu, na nyingine hazitatozwa kodi kabisa. Badala ya kuwafanya wananchi wa kawaida masikini kwa kuwatoza kodi nyingi, tutaruhusu watu watoe michango ya hiari kusaidia taasisi za umma. Serikali na wananchi pamoja tutalijenga taifa letu kwa moyo wa kizalendo.

Kupigana na RUSHWA tutaimarisha taasisi za sheria nchini kwa kuinua kiwango cha mishahara kwa watumishi katika taasisi zote za kisheria. Polisi hali yao ya maisha itainuliwa na nyumba wanazoishi kufanyiwa ukarabati na mpya kujengwa haraka kukithi mahitaji yao ya nyumba. Suala la familia mbili au tatu kushiriki chumba kimoja litakuwa historia katika kikosi cha polisi.

Majeshi yetu yatarekebishwa kutoka yale yanayongojea vita mpaka kuwa mahali pa kufikiri na kugundua vitu kwa ajili ya ujenzi wa Taifa. Pia mishahara yao itarekebishwa ili ikithi mahitaji yao ya kila siku. Majaji nao wataongezewa mishahara ili iwe vigumu wao kupokea rushwa na kupindisha ukweli mahakamani. Tunajua hakuna kiasi cha pesa kinachotosha mwanadamu akose vishawishi, lakini kwa kiasi kikubwa tutapunguza rushwa katika taasisi zetu za kisheria.

Mipango yetu itakuwa ya kudumu na hakutakuwepo na  oparesheni za kushitukiza ambazo ni sawa na kuhamisha rushwa kutoka taasisi moja kwenda nyingine. Pia wote watahesabiwa ni wananchi wa Tanzania bila kujali walihusika vipi katika serikali ya CCM iliyokuwepo madarakani. Kifupi hatutapoteza muda kwa yaliyopita bali tutakaza mwendo kwa yaliyo mbele yetu.

Tunajua kuna watu wenye majumba makubwa waliyojenga kwa pesa za rushwa walipokuwa madarakani, Lakini serikali yetu haitawabomolea watu hao majumba kwa kisingizio kwamba zilijengwa kwenye sehemu za barabara, Badala yake tutawaonyesha jinsi mtu anavyoweza kuwa tajiri kihalali bila rushwa au kuwathulumu wengine. Kwao hilo litakuwa somo kubwa maishani kujifunza. Kwa hiyo badala ya kuanza kukimbiza pesa zao nje wakidhani serikali yetu itawanyanganya kama walivyonyanganya, Watulize roho.

Pesa ni za watanzania. Wakizitumia Tanzania ni bora zaidi kuliko wakizipeleka nje ya Tanzania. Hapo washike neno langu. Mimi siyo mtu wa kuyatafuna niliyokwisha sema.



Kuhusu ELIMU tayari watanzania mlizoea elimu ya bure ambayo ilizalisha wasomi duni. Serikali yetu itaruhusu ushindani katika sekta ya elimu ili ubora wa elimu udumishwe. Taasisi za kidini na zile za watu binafsi zitaruhusiwa kuendesha mashule lakini kwa utaratibu urtakaowekwa na serikali yetu. Moyo wa kujitolea kutoka kwa wananchi pamoja na serikali, utahakikisha kwamba hakuna mwanafunzi wa Tanzania anayekosa elimu kwa sababu tu wazazi ni masikini hawawezi kulipa gharama za shule. Huo utaitwa moyo wa ENZI MPYA.

MATIBABU nayo yatakuwa sawa na elimu. Lakini kila juhudi zitafanywa kuhakikisha hakuna anayefukuzwa kwenye hospitali kwa kisingizio cha kukosa malpo ya hospitali. Serikali itakuwa bega kwa bega na taasisi za kibinafsi pamoja na zile za kidini. kuwahudumia wananchi wa Tanzania kiafya na kielimu. Mahospitali yaliyoko yataimarishwa na mengine mapya kujengwa. Pia vifaa vya kiafya vitaboreshwa kuyafanya mahospitali yetu yaweze kuwahudumia watu wa aina zote.

Hali ilivyo sasa mahospitali yetu yameachwa kiholela kwani wakubwa hutibiwa hata mafua nje ya nchi. Mamilioni yanayotumika kuwatibu viongozi nje ya nchi yanaweza kabisa kutumika kuyaboresha mahospitali yetu , Na hata kujenga mengine mapya.

Kwa mfano matibabu ya Mheshimiwa Mkapa hivi karibuni, Yameligharimu Taifa mamilioni ya shilingi kama siyo mabilioni. Hawatasema gharama halisi kuogopa aibu, Lakini watafiti wanasema ni kitita cha pesa.

Ajabu ni kwamba aliyofanyiwa huko, yangewezekana kabisa kufanyika nchini pamoja na hali duni za hospitali zetu. Mimi siyo muuguzi, lakini najua upasuaji unahitaji dawa ya kumfanya mtu alale ili kisu kiingie bila mgonjwa kusikia. Je dawa hiyo hapa nchini hakuna? Na kisu je, hata hicho hatuna?

Wengine wanasema Mkapa ni BONGE LA JITU Tena mtumiaji mzuri wa vileo kwa hiyo pengine dawa zetu za kumfanya alale zisingefua dafu. Sawa. Kama tunaweza kumfanya Tembo mzima alale na ahamishwe kutoka Ziwa Manyara hadi Ngorongoro, Je hata hiyo Mkapa angewekewa dozi moja asingelala?

Wengine wanasema hatuna madaktari bingwa wa kuweza kumhudumia RAIS. Mbona basi aliandamana nao huko alikotibiwa? Au walienda kufanya nini? Kuwatizama mabingwa wenzao wa nchi za nje  wakimhudumia rais wao? Kuna malalamiko kutoka baadhi ya madaktari bingwa nchini kwamba viongozi wanawapuuza wakati wana elimu sawa na ya wenzao wa nchi za nje.

Wanadai kwamba elimu ya udaktari haina njia fupi kwa daktari wa Amerika na yule wa Tanzania. Wote inabidi wapitie mafunzo mamoja na kuhitimu kumoja. Tatizo ni kwamba wenzetu wana nyenzo za kisasa wakati Tanzania tunatumia nyenzo za kizamani.

Lakini pia wanaliona hilo siyo tatizo kubwa kushindwa kulishughulikia tatizo kama la Mheshimiwa Mkapa nchini. Japo hawakutaka kutajwa, walijigamba kwamba wakati wa ajali ya TRENI Dodoma, walihusika katika kuwahudumia majeruhi waliokuwa katika hali mbaya mara kumi ya Mkapa na wakapona kabisa.

Hawaoni sababu yeyote ya Rais kutumia pesa za walipa kodi nyingi kiasi hicho kufanyiwa kile ambacho wenyewe wangeweza kukifanyia hapa nchini kwa gharama ndogo. Kuongezea uzito hoja yao wanasema, mbali na vyombo vya kisasa, dawa za kutuliza maumivu ni zile zile walizo nazo hapa nchini. Hata zile za kuzuia INFECTION nazo hazina tofauti na zile walizo nazo Tanzania.

Tofauti ni kwamba kwa sababu Mkapa ameziacha dawa hizo Tanzania, Amekwenda kulipa mamilioni kununua kile ambacho angeweza kukipata kiurahisi Tanzania.

Mwisho walimalizia kwa kusema kwamba haijalishi ni dawa gani utakazotumia. Kama nguvu ya mwili kupambana na madadhi imekufa, madaktari wanaweza kufanya sufuri kumfanya mgojwa apone.

Walisisitiza kwamba dawa husaidiana na mwili kupambana na maradhi. Walidokeza kwamba watu wengi wanakufa kwa magojwa yanayotibika kwa sababu uwezo wa kupambana  na maradhi mwilini umekufa. Walitumia lugha ya kitaalamu na kusema Upungufu wa Kinga Mwilini {UKIMWI} unawamaliza wengi japo dawa na mashine za kisasa wanazo.

Walionya kwamba viongozi wetu wanatakiwa waige mfano wa Rais wa Kwanza Kenya Mzee Jomo Kenyatta ambaye asliwaamini madaktari wa nchi yake na hakwenda ngambo kutibiwa. Alikufa usingizini Mombasa alipokuwa amekwenda kusheherekea sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya. Alikufa kishujaa nchini mwake chini ya uangalizai wa madaktari wazalendo wa Kenya.

Tanzania inawadhalilisha madaktari wake na kuonekana duni mbele ya wenzao wa ULAYA, lakini bado viongozi wetu wanakufa wakiwa mikononi mwa mabingwa hao. Walitoa mfano wa Nyerere kama kiongozi wa Tanzania aliyewahikufa mikononi mwa madaktari bingwa wa nchi za nje. Wanadai kwamba hata kama wanatoa mawazo wakati mgonjwa yuko nje ya nchi, Mawazo yao hayasikilizwa, jambo linaloleta lawama baadaye kwamba kama wangesikilizwa pengine Nyerere angekuwa hai leo.

Mambo hayatakuwa hivyo katika serikali ya ENZI MPYA. Tutaheshimu madakrari wetu, na watapewa kila motisha kuyaokoa maisha ya watanzania na viongozi wake wa ngazi zote. Hakuna sababu ya kutumia pesa za walipa kodi kuwaelimisha madaktari ambao kazi zao hazithaminiwi na viongozi.

Ndio maana wengi wa madaktari kutoka Tanzania wamehamia huko wanakokimbilia viongozi kwa matibabu. Inaelekea siku moja watakutana nao huko kama madaktari bingwa kumbe ni wale wale kutoka Tanzania na elimu ile ile waliyoidharau viongozi wetu.

Kuna wengine wanaohoji kwamba viongozi ni watu muhimu katika taifa na ni lazima kila hatua zichukuliwe kuchunguza afya zao.  Hatuipingi hoja hiyo, ila tunasema yote hayo yafanyike Tanzania..

 Wanataaluma hiyo wapo. Kwa nini viongozi waharibu pesa tunazozihitaji zaidi kwa yale yanayowezekana hapa? Kama ni ajali na iwe kiongozi kapoteza sehemu ya ubongo, halafu wajaribu kurudisha waliouokoteza chini zoezi hilo liwashinde, Hapo itaeleweka watakapotumia ndege yeyote hata kama ni ya jeshi kumkimbiza kiongozi husika kunakoweza kupatikana msaada wa haraka.

Lakini suala la Mkapa ni tofauti kabisa. Hata kama angehitaji vipimo vya mifupa vifanyiwe nje ya nchi, ilikuwa rahisi.Upasuaji ungefanyiwa Tanzania, na sehemu ya mfupa ipelekwe nje ya nchi kwa ucvhunguzi zaidi na majibu yangekuja mapema. Bado Rais angekuwa Nyumbani, angekunywa uji wa mbege kusaidia kujenga mifupa, na watu wangemuona kirahisi MUHIMBILI au IKULU kumtakia dua apone haraka.

Yale aliyokataa kuyafanya ndiyo anayoyafanya sasa. Bado inasemekana hajapona kabisa, na dawa bado anatumia tena kwa wingi. Nitashangaa zaidi nikisikia kwamba bado dawa anaagiza ngambo wakati zipo hapa TZ. MENGINE BAADAYE.


   
Munishi



Group: Members
Posts: 77
Joined: Nov. 2003

Posted: Dec. 23 2003,14:53   


http://munishi.com/

UWAZI UMERUDI TENA?

Mzee uwazi naona umekasirika ukanimwagia UMOMBO hapo mpaka mengine sikuelewa. Darasa la saba nafikiri ni mimi tu hapa. Wengine kama mimi sijui wako wapi.

Kama kiwango cha darasa la saba ni kina Munishi, basi waliofika kidato cha nne tanzania wako viwandandani wakiunda magari ya  Kitanzania, na wenzao waliobahatika kufika chuo kikuu basi watakuwa wakiunda ndege za Kitanzania.

Kumbe hapa ni watu wa kiwango cha darasa la saba tupu?

Lakini nakuomba unifafanulie pale ulipokuwa ukiwaambia waache kunipotezea muda wangu kwani elimu yangu nimeipata kwa njia ngumu sana. Eti ulisema niwatupe kapuni, au niwapuuze? Hapo sikubaliani na wewe mzee UWAZI.

Siwezi kuwadharau kwani huwezi kuelimika kama hakuna wasioelimika. Kipimo cha elimu kinapimwa na wale wasioelimika. Wakikosekana kama unavyonitaka niwatupe kapuni, hata mimi siwezi kusema nimeelimika. Uongo ni uongo kwa sababu kuna ukweli. Kama hakuna uongo, ukweli utakuwepo kufanya kazi gani?

Giza na nuru hazikai pamoja, lakini kila mmoja anamhitaji mwingine ndipo aendelee kuwepo. Kazi ya NURU itakwisha siku giza litakoma kuwepo. Siwezi kuwapuuza hata kama hawana elimu ya kiwango changu, lakini nawahitaji kuonyesha kiwango changu cha elimu. Bila wao mimi sina elimu. Na hata hivyo elimu yangu itafanya nini bila watu kama UWAZI kuwepo?

Au ulikuwa unamaanisha nini uliposema hivyo? Pole kwa usumbufu lakini niandikie kwa kiswahili nikupate sawasawa Mzee UWAZI

   
wabusara



Group: Members
Posts: 27
Joined: July 2003

Posted: Dec. 24 2003,00:23   

kasisi munishi,
wacha hotuba maneno mengi ya nini? tunasoma hizo riwaya zako mpaka tunasinzia. jaribu kufupisha kile unachokusudia kutueleza ili tukuelewe vinginevyo itakuwa sawasawa na kutia maji kwenye pakacha!!

   
Munishi



Group: Members
Posts: 77
Joined: Nov. 2003

Posted: Dec. 24 2003,14:05   


http://munishi.com/

SIKATI TAMAA KAZI KUBWA MBELE YANGU

Wanajiita wasomi kumbe mabomu. Bongo zao ni nzito kuelewa mambo. Inanibidi nitumie nguvu ya ziada kujieleza. Bora nifanye hivyo, wasiponielewa vizazi vijavyo watakujaelewa nilikuwa nasema nini. Siyo makosa yao. Walikulia na kusoma katika utaratibu uliowafanya mateka wa kufikiri. Wote wanafikiri kwa muelekeo mmoja. Ni sawa na roboti. Walitengenezwa hivyo. Kuliko kushinda nikijaribu kuwabadilisha, Bora kuinua kiwango cha elimu Tanzania ili tupate watu huru kufikiri.

Sasa nimejua kwa nini Mkapa anauza kila kitu Tanzania kwa mabepari. Pengine amejaribu kuwaamsha watanzania na akaona wako kwenye usingizi mzito.  Je nimsifu kwa kufanya alivyofanya? Hapana.  Kosa la Mkapa ni kuwaacha walivyo na akauza nchi kwa watu shapu kufikiri. Alikosea sana kwani naye alichangia katika kuwafanya watanzania walale katika usingizi mzito wa ujamaa chini ya CCM baba na mama. NItaandika mengi niwezavyo kwani nina uchungu sana na watanzania wenzangu waliolala usingizi mzito namna hii wakati huu wa ulimwengu wa sayansi na teke linalokujia. Sitachoka kuwaamsha, Ni ndugu zangu. Najua walipewa dawa gani kuwafanya walale. Nimepata dawa ya kuwaamsha. Ajabu hawataki hata kunywa dawa yenyewe.

Ni kama inakatisha tamaa. Lakini siyo Munishi akate tamaa ya kuwaamsha ndugu zake Watanzania. Wacha nijaze pakacha maji, lakini iko siku litajaa. Kila juhudi kuziba pakacha zinafanywa.

Muwe na Krismasi na mwaka mpya wa mafanikio kila mmoja wenu.


   
Munishi



Group: Members
Posts: 77
Joined: Nov. 2003

Posted: Dec. 24 2003,18:46   


http://munishi.com/

HERI NJEMA YA KRISMASI NA MWAKA MPYA WENYE MAFANIKIO TELE

Mathayo 2:1-18 Yesu alipozaliwa katika Bethlehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, Tazama Mamajusi wa mashariki walifika Yerusalemu, wakisema, Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? Kwa maana tuliiona nyota yake mashariki, nasi tumekuja kumsujudia. Basi Mfalme Herode aliposikia hayo, Alifadhaika na Yerusalemu pia pamoja naye. Akakusanya wakuu wa makuhani wote na waandishi wa watu, Akatafuta habari kwao Kristo azaliwa wapi? Nao wakamwambia, katika Bethlehemu ya Uyahudi, Kwa maana ndivyo ilivyoandikwa na nabii, Nawe Bethlehemu, katika nchi ya Yuda, Hu mdogo kamwe katika wajumbe wa Yuda. Kwa kuwa kwako atatoka MTAWALA atakayewachunga watu wangu Izraeli.

7 Kisha Herode akawaita wale mamajusi faraghani akapata kwao hakika ya muda tangu ilipoonekana ile nyota. 8 Akawapeleka Bethlehemu, akasema, Shikeni njia mkaulize sana mambo ya mtoto. Na mkiisha kumuona mniletee habari, ili mimi nami niende nimsujudie.

9 Nao waliposikia maneno ya mfalme, walishika njia na tazama, ile nyota waliyoiona mashariki ikawatangulia, Hata ikaenda kusimama juu ya mahali alipokuwapo Mtoto.10 Nao walipoiona ile nyota walifurahi furaha kubwa mno.11 Wakaingia nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye. Wakaanguka wakamsujudia, Nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu, dhahabu na uvumba na manemane. 12 Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, Wakaenda zao kwao kwa njia nyingine.

13 Na hao walipokwisha kwenda zao, Tazama, malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto, Akasema. Ondoka umchukue mtoto na mama yake, ukimbilie Misri, ukae huko hata nikuambie, kwa maana Herode anataka kumtafuta Mtoto amwangamize. 14 akaondoka akamchukua mtoto na mama yake usiku akaenda zake Misri.15 Akakaa huko hata alipokufa Herode, ili litimie neno lililonenwa na Bwana kwa ujumbe wa nabii, akisema. Kutoka Misri nalimwita mwanangu.! 16 Ndipo Herode alipoona ya kuwa amedhihakiwa na wale Mamajusi, alighadhabika sana. Akatuma watu akawaua watoto wote wanaume waliokuwako huko Bethlehem na viungani mwake mwote. Tangu wenye miaka miwili na waliopungua, kwa muda ule aliouhakikisha kwa wale mamajusi.

17 Ndipo lilipotimia neno lililonenwa na nabii Yeremia akisema.18 Sauti ilisikiwa Rama, Kilio na maombolezo mengi.Raheli akiwalilia watoto wake, Asikubali kufarijiwa kwa kuwa hawako. 19Hata alipofariki Herode, Tazama Malaika wa Bwana alimtokea Yusufu katika ndoto huko Misri, 20 AkasemaOndoka umchukue mtoto pamoja na mamaye ushike njia kwenda nchi ya Israeli kwa maana wamekufa walioitafuta roho ya mtoto.21 Akaondoka akamchukua mtoto na mamaye, akafika nchi ya Israeli. HILO NI NENO LA MUNGU KAMA LILIVYOANDIKWA KATIKA KITABU KITAKATIFU CHA MUNGU BIBLIA. AMEN.

Ndugu zangu wapendwa mabibi na mabwana. Tunaposheherekea kuzaliwa kwa Yesu, ni muhimu tuyatafakari kwa makini yote yaliyoambatana na tukio hilo. Kwanza ni furaha ya Mamajusi walioongozwa na nyota hadi alikozaliwa mtoto Yesu. Walifurahi sana, wakaanguka kumsujudia na kumtolea zawadi za dhahabu uvumba na manemane.

Pili ni unafiki wa  mfalme Herode kuwatumia mamajusi hao hao kumletea habari za alikozaliwa Yesu. Siyo kwa lengo la kufurahia kuzaliwa kwake ili amwabudu, bali alichukizwa na alitaka  ajue alikozaliwa ili amwangamize. Herode alikuwa mwanasiasa. Ilimbidi awatumie mamajusi wamfanyie uchunguzi wa wapi alikozaliwa Yesu kwa sababu askari wake wasingeweza kuufanya uchunguzi huo. Suala zima lilikuwa la Kiungu, na lilihitaji wataalamu wa nyota kujua wapi Mwokozi angezaliwa. Mambo ya Kiungu kwa wanasiasa kitendawili wanachomhitaji Mungu awategulie. Lakini Mungu hawezi kujichunguza mwenyewe ili ajiangamize. Mamajusi waliitii amri ya Mfalme, na walikuwa tayari kufanya kama Herode alivyotaka bila kujua madhara yake kwa Yesu.

Walifanya vyote. Walimtii Mungu na pia waliitii mamlaka ya wakati huo kama biblia inavyotufundisha. Lakini walipofikishwa mahali ambapo ingewapasa kuchagua nani wa kutii kati ya mamlaka na Mungu, wao walichagua kumtii Mungu kuliko Herode. Walipofika mahali ambapo Mwokozi wetu Yesu alikuwa amezaliwa, mawazo yao yalikuwa wamrudie Herode wampashe habari.Mamajusi hawakuijua nia ya Herode sawa na tusivyojua nia ya dunia kusheherekea Krismasi kwa vishindo kila mwaka. Kila mtu ana nia tofauti, na Mungu pekee ndiye anayejua nia ya kila anayesheherekea kuzaliwa kwa Yesu Leo.

Lakini Malaika wa Mungu aliwatokea katika ndoto na kuwaonya wasijaribu kurudi kwa Herode. Waliijua hatari ya kufanya hivyo, lakini walimtii Mungu. Hatua yao ilimkasirisha sana Herode, na ilibidi aamuru watoto wote wa kiume kuanzia miaka miwili kwenda chini wauawe.

Jambo lililopaswa kuwa la siri kati ya Mungu Malaika, Nyota na Mamajusi, likamhusu kila mtu baada ya mwanasiasa Herode kuingilia kati. Waliuawa watoto kutoka katika kila dini, ndiyo maana sishangai Krismasi inaposheherekewa na watu wa dini zote. Tukio lililokusudiwa kuleta furaha duniani, shetani akaligeuza likawa kilio. Nyumba nyingi zililia kwa watoto wao wa kiume kuuawa kulingana na amri ya Herode.

Pia usisahau kwamba Mungu alimwamuru Yusufu amchukue mtoto pamoja na mamaye wakimbilie Misri. Na hii ni baada ya kuhangaika siku nzima akitafuta nyumba ili mtoto azaliwe. Ilikosekana Nyumba yenye nafasi kwa Mwana wa Mungu kuzaliwa, lakini nyumba za anasa hazikosekani duniani. Ukiangalia kwenye TV yako utashangaa Yesu anatafuta pa kuzaliwa na wengine wanavunja nyumba za mamilioni ya pesa zianguke chini. Si bora wangeacha kwanza Mwokozi azaliwe ndani na kama kuzibomoa wabomoe baada ya Yesu kuzaliwa?

Mariamu ndiyo kwanza alikuwa amejifungua mtoto wa Kiume kwa uwezo wa kiungu, lakini alijifungua kama wanadamu wengine. Hapa ni mama aliyehitaji mapumziko, lakini ilibidi aanze safari ya kuwa mkimbizi wa kidini Misri. Tena hapa ni mtoto ambaye ndiyo kwanza ameingia ulimwenguni, na wazazi wanaanza safari usiku na baridi kali jangwani. Sijui nisemeje hapo. Nani alikuwa akichanganya dini na siasa hapo? Herode au Yesu mwana wa Mungu? Na je wakati huo Yesu kule Misri angeitwa mkimbizi wa kisiasa au kidini?

Krismasi ya kwanza ikachanganyika furaha na huzuni. Pengine ndiyo maana kila mwaka wakati wa sikukuu ya Krismasi shetani huangamiza watu kwa ajali barabarani.

Sitaki kumtukuza shetani, ndiyo maana nasema kwamba wale wanaoongozwa na Mungu wataziona hila za shetani na kuziepuka. Siyo lazima uumie na kuhuzunika wakati kuzaliwa kwa Yesu kunamaanisha furaha ya kweli moyoni.  Ukiyajua yote hayo, utajijua wewe unaisheherekea sikuku hii katika kundi gani.

Usijali kama tarehe 25 mwezi wa 12 ndiyo tarehe halisi ya kuzaliwa kwake, La Muhimu ni kwamba kweli Yesu alizaliwa. Pia usijali jinsi watu ulimwenguni kote wanavyosheherekea kwa nia na maana zao, bali jiulize wewe una nia gani. Ikiwa nia yako ni ili umwabudu na kukubali afanye kile kilichomfanya azaliwe, yaani  azaliwe moyoni mwako awe Mwokozi wako  binafsi, una heri. Tumuombe Mungu atufunulie siri iliyofichwa katika kuzaliwa kwa Yesu. Mwisho nawatakia Kismasi ya fanaka, Pamoja na mwaka mpya wenye mafanikio.

   
Munishi



Group: Members
Posts: 77
Joined: Nov. 2003

Posted: Dec. 30 2003,17:43   


http://munishi.com/

UWAZI UNATIA AIBU HAPA

Baada ya sikukuu nimerudi. Kuna kiumbe humu ndani kwa jina la UWAZI, nimemvumilia sasa basi. Kama ananisikia nina haya ya kumwambia.

Sasa umezidi. Unanitusi ni vibaya hivyo. Mimi kusema nataka kuwa rais wa Tanzania ni haki yangu. Wewe haki yako ni kumtafuta rais wa Tanzania.  Kama unaniona mimi sifai pia ni haki yako. Lakini usinitukane.

Mimi simtafuti nani anayefaa kuwa rais wa Tanzania, kwani namjua. Ni mimi mwenyewe. Ninafaa na ninajua hivyo. Siombi kura kwa wana ukumbi, bali nautumia ukumbi kuomba kura kwa watanzania milioni arobaini.

Ikiwa wanaukumbi watakuwa wamoja wa kunipatia kura, kila la kheri. Ikiwa wote watanipinga haitamaanisha wananchi milioni arobaini wamenipinga. Uwazi na wenzake mkome kufikiri kwamba mbinu zenu zitanikatisha tamaa kuingia ikulu.

Nina sifa za kuongoza na Uwazi na wenzenu mna sifa za kuongozwa. Hiyo ndiyo tofauti kati yetu.

Inasikika vibaya, tena inaonyesha picha mbaya kama matusi yataanzia kwako wewe unayejiita msomi.

Wengi wanaosoma  katika ukumbi huu watashindwa kukuelewa wewe ni msomi wa aina gani kama utaendeleza tabia zako za matusi humu.

Pengine watakuelewa baada ya kusoma post zako za kiingereza ambazo unasikika kama unaandika Kisukuma badala ya kiingereza. Kwa nini usiandike KISUKUMA kabisa badala ya kujidanganya na kutudanganya kwamba unajua kujieleza kimaandishi kwa kiingereza?

HAPA NI UPUMBAVU WAKO ULIOUANDIKA NA WENGI HAWAKUUELEWA

"Mkandara

U never stop amaze me! Ur statistics comparison leaves much to be desired. First u should know that there three kinds of lies, 1. Lies, 2. #### lies and 3. Statistics. I'm sorry to say this but ur using statistics to lies us.

What are ur take about these :-)

Let's call a spade a spade. Tanzania ni mojawapo ya nchi FUKARA sana duniani. Tanzania imekuwa grouped katika nchi zinazoitwa HIPC (HIGHLY INDEPTED POOR COUNTRIES) mwenye tafsiri yake kwa kiswahili anisaidie. Majority (> 50%) of Tanzanians live below poverty level, spending less than $ 1 per day. Sasa kama bado unabisha kuwa Tanzania sio nchi masikini, then I've to rest my case.

Mimi sitegemei Rais mtarajiwa kufanya MIRACLES kututoa from HIPC kuwa DEVELOPED COUNTRY. That's utopia and I'm not utopian."

Eti hapo msomi amejikakamua kujieleza kwa kiingereza

Ulivyo mjinga, nilipokuambia umetumwagia umombo hata hatuelewi, wewe ulifikiri kwamba nilikusifia. Sasa imekuwa tabia yako kuandika Kisukuma humu ndani ukifikiri ni kiingereza. UNAJIAIBISHA, ACHA MARA MOJA.

   
Mtanzania



Group: Members
Posts: 4
Joined: June 2003

Posted: Dec. 31 2003,06:41   

Munishi ananikumbusha mtoto mdogo ambaye amepewa toy la gari. Kila wakati utamkuta nalo akilichezea.  Naona internet imekuwa kama toy (la mtu mzima) kwake kwa jinsi anavyoweka mapicha yake kila apatapo nafasi. Aibu na Kichekesho  :D

   
Munishi



Group: Members
Posts: 77
Joined: Nov. 2003

Posted: Dec. 31 2003,11:40   


http://munishi.com/

TUNAKUJUA MZEE MKAPA TUMIA JINA LAKO

Mzee MKAPA unayejiita MTANZANIA umepona? Mbona sikusikii kabisa mzee?  Jitokeze hata kama utakuwa kwenye machela mradi unapumua haina neno. Tatizo lako ulifikiri magonjwa ni ya wengine tu. Ndiyo maana hutaki kabisa kuonekana hadharani ukiwa mgonjwa. Lakini ukikataa kuonekana ukiwa mgonjwa si ukiaga tutakupa heshima za mwisho pale uwanja wa Taifa?

Jitokeze mzee ugonjwa ni wa kila mtu. Tembea hata na MAGONGO usijali. Ulifikiri umempa nini Mungu ili usiugue kabisa? Mungu hapokei rushwa. Pengine ungemkatia lile pande la dhahabu lakini hapokei kwani dhahabu ni mali yake Mungu.

BAADA YA MKAPA NI MUNISHI

Sitaki huruma za Mkapa ili niwe Rais. Ninachotaka ni KATIBA mpya kabla ya uchaguzi. Watanzania tutakosea sana kuingia kwenye uchaguzi bila katiba mpya. Hakutakuwepo mabadiliko hata kama rais atakuwa Bush kutoka marekani. Moja mara sufuri ni sufuri. Elfu kumi mara sufuri bado ni sufuri. Uchaguzi bila katiba mpya ni sufuri.

Tanzania inataka mapinduzi. Tuipindue serikali ya CCM, ili tuwe na serikali mpya. Mimi nitaipindua serikali ya CCM. Sitaipindua kijeshi, bali nitafanya hivyo kwa kuwaasa wananchi wa Tanzania wasiingie kwenye uchaguzi bila ya katiba mpya. Wakifanya hivyo, haijalishi matokeo, Lakini itakuwa sufuri. Munishi kuwa rais chini ya katiba ya sasa, SITAKI. Ningekuwa nataka hivyo ni rahisi sana. Ni kiasi cha kujiunga na chama chochote cha kisiasa na kugombea URAIS. Nafasi hizo ziko nyingi na nimekataa mialiko mingi ya kuwa mgombea katika utitiri wa vyama vya upinzani.

Mapungufu yaliyoko katika katiba yetu, Yatamzuia kiongozi yeyote kuleta mabadiliko ya maana Tanzania. Madaraka ni sawa na kileo. Huwezi kunywa pombe nyingi ukose kulewa. Katiba yetu inampa Rais madaraka mengi, na hakuna atakayekuwa rais chini ya katiba ya sasa akose kulewa madaraka. CCM wanajiita Chama Cha Mapinduzi, Lakini nitawapindua. Nyerere alijua kwamba siku moja watakuja watu kama kina Munishi watake kuipindua serikali ya CCM, ndiyo maana aliwahi mapema kukiita chama cha TANU CCM japo hakijampindua yeyote. Aliona mbali, akakibandika chama jina la MAPINDUZI kujihami kupinduliwa. Lakini hana bahati kwani Watanzania tumeamua kuwa na mapinduzi ya kweli, nayo ni kuipindua serikali ya CCM baada ya kuipindua KATIBA.

   
Mkandaraha



Group: Members
Posts: 3
Joined: Dec. 2003

Posted: Dec. 31 2003,13:07   

MKAPA NA MUNISHI WAPATANISHWE

Malumbano yanayoendelea kati ya Mchungaji Munishi na Mheshimiwa Rais Mkapa siyo mazuri kwa nchi yetu. Afrika tunajua kuitisha mikutano ya upatanishao wakati damu nyingi sana imeshamwagika. Hatuna hekima ya kuzuia kabla ya madhara makubwa kufanyika. Mizozo yote huanza na malumbano kama haya mnayoyaona hapa. Kila upande ukidai kunyimwa haki na upande wa pili. Tusipoziba ufa hapa tutajenga ukuta. Malumbano yakizidi na yakomae kabisa, huzaa magomvi ambayo nayo huzaa vita.

Hakuna vita inayoanza kama vita.  Huanza kama maneno ya chokochoko kama hizi mnazozisikia hapa. yasipozimwa au kupatanishwa huzaa vita. Ni muhimu sana kuwapatanisha Mheshimiwa Mkapa na Mchungaji Munishi. Nionavyo mimi Munishi hana historia ya kulumbana na serikali. Malumbano yalianza pale serikali ilipoipiga marufuku kanda toleo la saba ya mchungaji Munishi. Sababu hasa zilikuwa kisiasa kuliko vinginevyo. Sijui serikali walisikia nini kwenye kanda hiyo na kuamua kuipiga STOP, Lakini mimi sioni chochote ndani ya kanda hiyo ambacho kingeifanya serikali kuhamaki kama ilivyohamaki.

Baada ya kukurupushani za kuweka watu ndani na habari za kutafutwa Munishi kusambaa, ndipo Munishi alipotoa taarifa kwa vyombo vya habari kwamba maisha yake yalikuwa hatarini kufuatia zoezi la serikali kuzikamata kanda zake. Sina data zaidi ya hapo, lakini nafikiri kuwa malumbano yalianzia hapo. Kama sikosei pia ndio sababu kubwa ya Munishi kuanzisha Web Site yake ambayo wengi tunaiona kama mahali pa kutolea malalamiko yake kuhusu hatua ya serikali. Anahisi kaonewa.

Serikali nayo kwa upande wake imeendeleza ukimya ambao siyo wa kawaida. Ni kama wanadharau. Kama kanda tulizuia na watu tukawaweka ndani, SO WHAT? Mtaifanya nini serikali yenye ridhaa ya wachache ambayo siyo butu? Kwangu msimamo huo hauisaidii serikali. Unathibitisha jinsi ambavyo viongozi wa Tanzania wanavyodhamini ubabe wa vyombo vya dola.Wanaweza kumfanyia mwananchi chochote na wasipelekwe popote. Hata kama simba aliumbwa ale nyama ya swala, lakini swala hawajui hilo. Ndio maana kila inapobidi, swala hutimua mbio. Vinginevyo kizazi cha swala mwituni kingekuwa kimemalizika. Kwamba swala bado wapo mwituni pamoja na wingi wa simba, hiyo inaonyesha serikali haina nguvu inazofikiri kuwa nazo.

Nashauri kwamba Munishi na Mkapa wakae pamoja kutatua tatizo ambalo linakua kila kukicha. Ubabe hautasaidia katika hili. Msisahau kwamba nchi za magharibi huifurahia mizozo ndani ya Afrika. Huitumia kama soko lao la kuuzia silaha. Ninachosema hapa ni kwamba ni rahisi sana kwa nchi za magharibi kutoa misaada ya silaha kwa yeyote anayeonekana mpinzani wa serikali. Siyo ajabu wakatumia mzozo huo kumpa mpinzani silaha bure, huku wakiidanganya serikali inunue silaha kwao kupambana na mpinzani. Mwisho wa kila kitu mnauana wenyewe, na silaha mnazilipa kwa njia moja ama ile nyingine. Tuyatatue matatizo yetu wenyewe. Tena kabla hayajatuletea madhara. Hii ni tathmini yangu mwenyewe kuhusu malumbano kati ya Munishi na Mkapa.

   
Binti Lishe



Group: Members
Posts: 68
Joined: Nov. 2003

Posted: Dec. 31 2003,13:40   

Jamani,

Huko nyuma mie nilidhani kwamba Munishi ni punguani, lakini kutokana na kumkemea na kukosoa kiingereza cha Uwazi nimegundua kwamba kumbe Munishi ana akili timamu kabisaa!  Sasa ndugu yangu Munishi kwa kuwa umeonyesha kuwa una akili timamu, tunaomba usikilize kilio cha wengi cha kufupisha maandiko yako na pia tunakuomba uache kutubandikia picha zako.  Imetosha!

Happy New Year guys!

Binti Lishe

13 Next Page