Munishi
Group:
Members Posts: 77 Joined: Nov. 2003
|
 |
Posted: Dec. 13 2003,16:54 |
 |

Watakuja na mioto wataondoka wamejiinamia kwa
huzuni. Kwao elimu ni kujua lugha ya kiingereza. Wanasahau hata hapa
tunasoma. Shule wao walimaliza, na wanajiita wasomi.
Wamendanganyika. Ukisoma wanayoandika hayafanani na shahada
wanazodai kuwa nazo. Elimu yao inatiliwa mashaka.
Kwao
mahali pekee pa kupata elimu ni darasani. Ni watu wa ajabu sana. JKT
iliingiza baridi kwenye bongo zao. Ni sawa na breki za gari
zilizoingiza hewa ndani. Ukikanyaga ukifikiri una breki utashangaa.
Gari haisimami. Lazima utoe hewa kwenye bomba linalopitisha mafuta
ya breki ndipo gari yako iwe na breki. Nyerere aliingiza hewa katika
bongo za wasomi wetu akitumia JKT. Alibaki mwenyewe mjuzi wa kila
kitu. Siyo ajabu waliimba ZIDUMU FIKRA ZA NYERERE. Walikuwa sawa.
Nani mwingine aliruhusiwa kufikiri Tanzania?
Woga ndio
uliotawala mawazo yao. Hawawazi kingine isipokuwa CCM aliyoanzisha
Nyerere na sasa imezeeka. Sera za ujamaa ziliharibu Tanzania na CCM
haifai kurudishwa madarakani. Sisi tunasonga mbele. Enzi mpya
Tanzania ni lengo letu. CCM sasa basi. Tuna hamu ya kuiona Tanzania
mpya bila CCM. Tanzania ni mali yetu watanzania na siyo mali ya CCM
na Mkapa.
 Nchi ya Tanzania ni mali ya watanzania wote na siyo ya
Mkapa na CCM kama inavyoekea kuwa.Vitendo vinavyofanywa na serikali
ya chama tawala CCM vinaonyesha wazi jinsi wanavyofikiri kuwa
Tanzania ni mali yao.
Kwamba serikali inaweza kuwaua raia
wake kwa sababu wana mawazo yanayotofautiana na chama tawala, siyo
tu ni kinyume na haki za binadamu, bali ni wendawazimu
uliochanganyika na upumbavu wa hali ya juu.
Nauita upumbavu
kwa sababu ni afadhali ungekuwa ujinga ambao unaweza kutoka wakati
mhusika anapoelimishwa. Lakini kwa kuwa yalifanywa na watu
wanaojiita wasomi tena wa vyuo vikuu, basi yanakuwa ya kipumbavu
maana hatujui wahusika wataenda chuo gani tena kuelimika ili wajue
kuwa katika dunia tunayoishi ni vigumu watu wote kukubaliana
kimawazo, hata kama mawazo hayo yanatoka kwa Rais wa
nchi.
Matata na chokochoko zilizoko duniani mara nyingi
huanzishwa na watu wanaojifanya kujua kila kitu, na kumbe hawajui
kwamba hawajui. Na Tanzania tuna Mkapa anayejifanya kujua kila kitu
na kumbe hajui impasavyo kujua. Matokeo yake ni kwamba Tanzania
itaigizwa kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe ambavyo havijawahi
kuonekana popote duniani.
Nasema itakuwa vita mbaya kwa
sababu karibu kila mtu Tanzania amepitia mafunzo ya kijeshi, kosa
alilolifanya Nyerere akifikiri kila mtu anapokuwa mwanajeshi ni
rahisi kumtawala mtu huyo.
Jeshini hawaulizi maswali, bali
wanatii amri. Ni kigezo hicho ndicho kilichomfanya Nyerere aamini
kuwa watanzania wakipata mafunzo ya kijeshi watakuwa na nidhamu, na
itakuwa rahisi kuwatawala. Alifanikiwa kuwatawala watanzania kwa
karibu miongo miwili bila ya vita vya wenyewe kwa wenyewe. Siyo
kwamba Tanzania haikuwa na matatizo, lakini alijua nini cha kufanya
yanapojitokeza tofauti na anavyofanya Mkapa ambaye anafikiri kila
tatizo linatatuliwa kibabe na kutumia nguvu za
dola.
Watanzania aliowatawala Nyerere ni wale wale Mkapa
anaoshindwa kuwatawala, tofauti ni kwamba Nyerere aliweza kuwaibia
watanzania bila wao kujua, wakati Mkapa anawaibia waziwazi. Nyerere
alikuwa akigundua wananchi wamemshtukia anawaomba msamaha wa geresha
wakati mkapa anamwamuru mkuu wa Polisi awashughulikie wote wanaokuwa
na mawazo tofauti na chama tawala. Nao Polisi kama 'Robots' na bila
kutumia ubongo wao wanawamiminia risasi za moto ndugu na dada zao
watanzania na kusababisha vifo ambavyo idadi yao haitajulikana
kamwe. Serikali inasema ni watu 23 tu, wakati chama cha upinzanini
CUF ambacho ndicho kilichoadhirika kwa wanachama wake kuuawa
kinasema watu zaidi ya 300 waliuawa kinyama na mamia kujeruhiwa huku
maelfu wakiwa wakimbizi wa kisiasa Mombasa Kenya kwa mara ya kwanza
tangu Tanzania ipate uhuru. Na yote hayo yamesababishwa na utawala
wa kimabavu wa dikteta Mkapa.
 Mkapa
aliamuru mauaji ya kutisha Zanzibar, na kufuta jina la Tanzania kuwa
kisiwa cha amani. Mwenyewe alikiri kwamba Tanzania imegubikwa na doa
kubwa jeusi.
Kinachoshangaza na kogopesha siyo idadi ya watu
waliokufa, bali tumefikia mahali ambapo Polisi wa Tanzania wanatumia
bunduki zilizonunuliwa na watanzania kuwaua watanzania. Mbaya zaidi
ni kwamba karibu watanzania wote waliokufa dini yao ni ya Kiislamu
jambo linalolielekeza tatizo lenyewe kuwa la kidini zaidi kuliko
kisiasa. Siyo kwamba likiwa la kisiasa pekee ni rahisi kulitatua,
maana sidhani Tanzania ya leo kuna mwanasiasa anayejua siasa za
kutosha kulitatua. Mkapa ni mtoto asiyekua kisiasa na siyo makosa
yake.
Nyerere baba yake kisiasa hakutaka akue ili awe
anamnywesha maziwa ya kisiasa kila siku. Alifikiri angekuwepo mpaka
azaliwe mtoto mwingine ambaye naye kama Mkapa, mpango ulikuwa kwamba
asiruhusiwe kukua bali aendelee kupewa maziwa ya kisiasa sijui
ingekuwa mpaka lini.
Lakini alisahau kuwa mwanadamu hawezi
kuishi milele duniani, ila mbinguni au motoni ndiko watu wanakoishi
milele.
Mungu alipoamua kumchuku Nyerere {na sijui alimweka
wapi,}Ndipo mambo yalipoanza kumharibikia Mkapa. Kama mtoto yatima
kisiasa, hakujua aanzie wapi amalizie wapi. Ninasikitika kusema kuwa
mpaka sasa Mkapa amechanganyikiwa kisiasa. Wanaojifanya kumshauri
ndio wanaoharibu zaidi. Inavyoonekana hatujui ni nani hasa
anaeiongoza Tanzania kati ya Mboma mkuu wa majeshi, Maita mkuu wa
Polisi, na Kingunge Nguoyambali Mwiru mshauri mkuu wa Mkapa.
Habari kutoka vianzio vyetu zinasema kuna uvutano mkubwa
kati hawa watatu kila mmoja akidai kuachiwa urithi wa Tanzania.
Mboma anadai kuwa Nyerere alimwambia alinde muungano kwa nguvu zote
na akiona kuna hatari ya muungano kuvunjika, Jeshi lichukue
madaraka. Kingunge naye anadai kuwa Nyerere alimwambia atumie busara
yote kuhakikisha siasa zinaendeshwa bila kumwaga damu ya Watanzania.
Naye mkuu wa Polisi anadai kuwa Nyerere alimwambia awafuatilie kwa
karibu wanasiasa kuhakikisha kuwa hawaiuzi nchi kwa mabepari wa
mataifa ya magharibi. Mkapa naye anadai kuwa Yeye ndiye aliyeachiwa
nchi kuhakikisha kuwa siasa ya ujamaa haifutiki Tanzania.
Ukiyaangalia madai yao, na uwe kidogo ulimfahamu Nyerere,
utakubaliana nao kuwa wote wanasema ukweli. Ni ukweli kwa sababu
mwalimu alitaka kuwaona kila siku Butiama wakilalamika kwaba hili
halitekelezeki kwa sababu linapingwa na lile. Yaani alihakikisha
kuwa la mkapa halitekelezeki kwa sababu linapingwa na Mkuu wa
Polisi. Na lile la Mkuu wa majeshi linakwamishwa na KINGUNGE
NGUOYAMBALI.
Wakati kila mmoja wao alipopeleka malalamiko
yake Butiama ndipo Nyerere alipata nafasi ya kuwaonyesha jinsi
walivyo wajinga, na inasemekana alikuwa akiwafundisha kama watoto wa
Nasari. Ndio maana wote wanamwita mwalimu. Ni kweli alikuwa mwalimu
wao.
Sasa Mwalimu hayupo, na wanafunzi wake wameanza
kuvurunda mambo.Tayari Polisi wamewaua raia zaidi ya 50 wasiyo na
hatia kwa madai kuwa walihudhuria mkutano wa kuda haki yao
waliyonyanganywa na Serikali.
Wanajiona kama hawana haki ya
kudai chochote katika nchi yao.Wakitafuta wa kulaumu wanamuona
Nyerere waliyemwita BABA.
Wanaona Nyerere alikosea kuwaachia
urithi watu wanne tu na kuwasahau watu milioni karibu 40 kutegemea
maamuzi ya watu wanne.
Matatizo yanayopikwa Tanzania sasa
hivi yana michango mingi iliyochangia kuyafikisha hapo yalipo,Lakini
Nyerere pamoja na kwamba ni marehemu hawezi kuepuka
lawama.Aliitawala Tanzania kama mali yake, na mawazo yake ndiyo
yaliyokuwa sahihi, Na hata kama aliweka Mtu, alihakikisha ni mjinga
atakayeketi miguuni pake siku zote kufundishwa.
Namkumbuka
Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi ambaye Nyerere alifikiri ni mjinga,
lakini baada ya kutawazwa kuwa Rais wa jamhuri ya muungano, alianza
kufanya vitu vyake kama mwanaume anayefikiri. jambo ambalo
lilimletea mikwaruzo na huyo aliyekuwa akijifanya kujua kila kitu.
 Kwa sasa kuna Mkapa anayeitwa Rais wa Tanzania, Lakini
nikienda Tanzania nitakutana na mzee Ali Hassan Mwinyi kwani kwangu
huyo ndiye mtu aliyethubutu kuwa na mawazo huru wakati wa Nyerere
kwenye uongozi wa Nyerere. Mkapa na wenzake wanatakiwa wajue kuwa
sasa Nyerere hayuko, na majukumu ya kuiongoza Tanzania lazima
yahusishe Watanzania wote.
Kiburi kwamba wao ndio walioachiwa
nchi waache. Hata huyo wanaedai kuwa aliwaachia Tanzania haikuwa
yake. Matatizo ya Zanzibar yatafutiwe uvumbuzi wa haraka
unaozingatia haki na siyo ubabe kama serikali inavyojaribu
kufanya.
Madai ya chama cha CUF kwamba uchaguzi urudiwe na
iundwe tume huru, pamoja na kubadilishwa kwa katiba yatiliwe maanani
kuinusuru nchi na vita vya kidini ambavyo vinaonyesha kila dalili ya
kuanza. Wakristo wasifurahi kwamba serikali ya Mkapa inawazibiti
Waislamu, wajue kuwa serikali hiyo hiyo inaweza ikawageukia na
wao.
Mkapa aache mara moja kuitegemea Amerika kumsadia
kutatua tatizo la Tanzania kwani sera za Marekani ni kuwanyanyasa
Waislamu duniani kote.Wananchi wa Tanzania wana uhuru wa kuamini
dini yeyote na ikiwa Wazanzibar wengi ni waislamu sioni sababu ya
wao kuadhibiwa kwa sababu ya dini wanayoiamini.
Hata kama
wanataka kuuvunja muungano kwa sababu wanazozijua wao, wawe huru
kufanya hivyo kwani ni kinyume kuwalazimisha kubaki kwenye muungano
ambao hawaoni faida yake.
Nyerere alipata sifa duniani kwa
kuunganisha Tanganyika na Zanzibar, na Mkapa atapata sifa ya
kutenganisha Zanzibar na Tanganyika kuepusha umwagikaji wa damu.
Kila kitu kina wakati wake. Wakati wa Nyerere ulikuwa wa
kuunganisha, siyo vibaya wakati wa Mkapa ukawa ni wa kutenganisha
kwa faida ya walio wengi.
Kumuenzi Nyerere siyo kumwaga damu
kutetea sera zake ambazo alizitetea bila kumwaga damu.
Mwisho
ni vizuri Mkapa akajua kwamba yeye siyo Nyerere, na kuna vitu
alivyoviweza Nyerere ambavyo yeye haviwezi. Pia asisahau kuwa kizazi
alichokitawala Nyerere ni tofauti kabisa na kizazi anachokiongoza.
Sura nzuri na maumbile ya Nyerere yalimsaidia kusamehewa
haraka na umma, Wakati sura ya kutisha na maumbile ya ajabu ya Mkapa
yanamfanya awe mtu asiyesamehewa haraka akikosa.
Tayari
Mkapa ameshaukosea umma wa Watanzania kwa kuamuru Polisi wawaue
zaidi ya watu hamsini huko Zanzibar, sijui itawachukua muda gani
kumsamehe. Lakini kama ningekuwa Mkapa, Ningejiuzulu niombe msamaha,
halafu niunde tume ya marekebisho ya katiba ili wananchi watoe
mawazo yao kuhusu jinsi wanavyotaka kuongozwa. Halafu wafanye
uchaguzi ndani ya katiba mpya. |